SISI NI WAPITAJI DUNIANI
SISI NI WAPITAJI DUNIANI
Shukrani kwa Mungu kwa nafasi
hii ya kutafakari habari njema.
Kama kichwa kinavyosema, wanadamu wote ni wapitaji ulimwenguni. Hatujapewa makao
ya milele hapa Duniani, lakini baada ya maisha ha ya kuna makao ya milele kwa kila
mwanadamu. Mtume Paulo anasema katika waebrania 13:14, “ Maana hapa hatuna mji (makao) udumuo, bali twautafuta ule ujao”.
Ni mji upi huo anasema wanautafuta au
wanatamani kuufikia. Ni mji au makao ya mbinguni, Ndivyo Yesu kristo alivyosema,
“maana naenda kuwaandalia mahali
(makao). Basi mimi nikienda na kuwaandalia
mahali, nitakuja (nitarudi) tena niwakaribishe kwangu ili nilipo mimi, nanyi mwepo”
Yohana 14:2. Yesu aliwaeleza wanafunzi wake juu ya makao ambayo anakwenda kuwaandalia
mbinguni.
Biblia inaeleza wazi kuhusu maisha
ya milele ya mwanadamu baada ya Dunia hii. Kuna makao ya aina mbili, Mbinguni-
katika Ufalme wa Mungu na Yesu kristo, na Jehanamu mahali pa mateso na hukumu
kwa wote waliomwasi Mungu, muumba wa Mbingu na nchi.
BIBLIA, Neno la Mungu linasema, Mungu atamhukumu kila
mwanadamu kulingana na matendo yake, wengine wataingia mbinguni – mahali pa
raha, furaha na amani, wengine wataingia Jehanamu mahali penye mateso makali na adhabu. Biblia inasema, “nikawaona
wafu wakubwa kwa wadogo, wamesimama mbele ya kiti cha enzi, na vitabu vikafunguliwa
na kitabu kingine kikafunguliwa ambacho ni cha UZIMA, na hao wafu wakahukumiwa kwa
kadri ya matendo yao. Na iwapo mtu yeyote hakuonekana ameandikwa katika kitabu
cha uzima, alitupwa katika ziwa la moto (Jehanamu)” – Ufunuo 20:12,13,15.
Hakuna mwanadamu anayetamani kukaa Jehanamu milele,
hata hivyo Neno la Mungu linasema, yeyote ambaye jina lake halikuonekana katika
kitabu cha UZIMA alitupwa katika ziwa
la moto. Inatisha mno kutupwa katika ziwa (bahari) la moto.Kitabu cha uzima kina majina ya
watu wamwaminio Yesu na kuyatenda mapenzi ya Mungu. Je jina lako lipo katika kitabu
cha Uzima?
Biblia katika Mathayo25:35-46 inaeleza Jinsi mwana wa
Adamu (Yesu kristo) atakavyorudi mara ya
pili ataketi katika kiti chake cha enzi, naye atawahukumu mataifa yote. Kila mwanadamu atasimama mbele zake (sisisote), naye atamhukumu
kila mmoja kwa kadri ya matendo yake. Wale waliotenda mema wataingia katika uzima
wa milele na waliotenda maovu wataingia katika adhabu ya milele. Ni jambo la
kutisha kuwa siku moja tutasimama mbele za Mungu kuhukumiwa, Biblia inasema “
kwa maana sisi sote tutasimama mbele ya kiti cha hukumu cha Mungu ……. na kila mtu atatoa habari zake mwenyewe
mbele za Mungu” – Warumi 14:10,12.
Kristo Yesu ndiye jibu pekee kwa maisha yetu wanadamu.
Anasema, “mimi nalikuja ili wawe na uzima
wawe nao tele” – Yohana 10:10. Yeye pekee ndiye anaweza kutufikisha mbinguni,
anasema “mimi ndimi njia ya kweli na uzima. Mtu hawezi kufika kwa Baba
(mbinguni) pasipo mimi” – Yohana 14:6.
Ni yeye pekee ndiye awezaye kumwokoa mwanadamu juu ya dhambi na hukumu ya mwisho.Yesu
alikuja ili kila amwaminiye asipotee/asiangamie bali awe na uzima wa milele.
Soma Yohana 3:16-19 Yesu hakuja duniani ili kuhukumu ulimwengu, bali wanadamu waokolewe
kupitia kumwamini na kumfuata yeye – (Yohana 3:17)
Biblia inasema, “amwamini yeye hahukumiwi,
asiyemwamini (Yesu) amekwisha kuhukumiwa” – Yohana 3:18.Yeye amwaminiye
Yesu anavuka kutoka mautini kwenda Uzimani.
Ndugu yangu, ikiwa unamwamini Yesu, ninakutia moyo songa
mbele katika kwa Jina la Yesu. Ikiwa haujampokea Yesu ,tambua kuwa pasipo yeye utahukumiwa
kwenda Jehanamu. Mkubali yeye leo, tubu dhambi zako na uishi kwa ajili yake.
Ili tuingie mbinguni ni lazima tuishi maisha matakatifu
na safi mbele za Mungu. Pasipo utakatifu, hatutaingia mbinguni. “Heri wenye moyo safi maana hao watamwona Mungu“
–Mathayo 5:8. Pia Paulo anatuagiza, “ tafuteni kwa bidii kuwa na amani na
watu wote na huo utakatifu ambao hapana mtu atakayomwona Mungu asipokuwa nao” –
Waebrania 12:14 Ni hatari sana kwa mkristo kuishi maisha ya dhambi, kwa kuwa
ataikosa mbingu.
Mbinguni ni mahali pazuri, pa furaha kuliko mahali pengine
popote. Tutamani kufika huko. Itazame mistari hii inayoeleza juu ya mbinguni, “ na mji ule ulikuwa wa dhahabu safi, mfano wa kioo” – Ufunuo 21.18; “ Na njia ya mji ule ni dhahabu safi kama
kioo kiangavu”- Ufunuo 21:21.Pia ufunuo 21:2,4 inasema, Nami nikaona mji ule mtakatifu, wala mauti haitakuwepo, wala maombolezo
….” Oh mbinguni pana uzuri usioelezeka, hakuna njaa, magonjwa wala matatizo
ya kiuchumi. Tuende sasa mbinguni, naam, kwa kutembea na Yesu tungali hai.
Jehanamu ni mahali pabaya
mno. Ni mahali penye moto usiozimika, unaowatesa watu milele na milele. Neno la
Mungu limeeleza juu ya Jehanamu kuwa ndani yake kuna kilio, maombolezo na kusaga
meno. – (Mat 13:42, 13:50, 25:30), Ni hatari mno.
Katika luka 16-18:-31, Yesu anaelezea maisha baada ya
kufa ya tajiri mmoja na Lazaro maskini. Tajiri aliishi maisha ya anasa na maskini
Lazaro alikuwa mcha Mungu. Baada ya kufariki kwao, Lazaro alichukuliwa hata mahali
tulivu penye utele (mbinguni). Lakini Yule Tajiri aliingia katika mateso makali
katika moto mkali. Mmoja alienda mbinguni na mwingine Jehanamu.
Hatima
ya maisha ya mwanadamu ipo mikononi mwake. Ikiwa atamwamini na kumtii Yesu ataingia
mbinguni, kinyume chake, hukumu ya kutisha mno, itakuwa mbele yake, yaani Jehanamu
ya moto.
Ndugu yangu, tusiipende dunia na anasa zake, tukiipenda
dunia na uovu wake, ni dhahiri tutaikosa mbingu. Yesu alisema, “itamfaidia mtu nini kuupata ulimwengu wote,
akipata hasara ya nafsi yake”- marko 8:37. Itakufaidia nini mwanadamu kuupata
ulimwengu na anasa zake, lakini
Ukaipoteza nafasi yako katika
adhabu ya milele!!!!
Yesu alikuja ili tuwe na uzima wa milele.
Mungu anatupenda sana wanadamu, hata akamtuma Yesu. Yesu Kristo, mwana wa Mungu
aliteseka msalabani kwa ajili ya dhambi zetu. Leo anatuita na kutukumbusha kuwa
inatupasa kumpenda yeye na kumtii ili atufikishe mbinguni. Hapendi mtu yeyote apotee,
bali awe na uzima wa milele.
Mungu akubariki kwa kusoma
ujumbe huu. Hayakuwa mawazo ya kibinadamu, au ujuzi wa akili, bali niNeno la
Mungu, llilo hai na kweli milele yote. Hivyo yaweke moyoni mwako, ukayatendee kazi.
Ikiwa haujampokea Yesu moyoni
mwako au ulirudi nyuma – ni muhimu kujikabidhi
kwa Bwana YESU, kiri maneno haya ukiamini moyoni mwako.
Bwana
Yesu, naja mbele zako, mimi ni mwenye dhambi. Ninaomba unisamehe, nitakase kwa damu
yako na uandike Jina langu katika kitabu cha Uzima. Ninakukaribisha moyoni mwangu
uwe Bwana na mwokozi wangu tangu sasa na hata milele. Amen.
Amini kuwa Yesu kristo ameingia ndani yako,
shirikiana na wale wampendao ili uweze kukua ndani mwake.
Mungu wa Mbinguni akubariki.
Kwa mawasiliano zaidi;
0759
895181/0713049601
Justo
Mathew.
Comments
Post a Comment